Saturday, March 27, 2010

Kwani Katika Siasa Agenda Yetu Sisi ni Ipi?

Nimejikuta napata msukumo mkubwa kutoka ndani yangu kulizungumizia swali hili baada ya tafakuri ya kina kwa muda mrefu takribani mwaka mmoja na zaidi. Katika swali hili napenda kuizungumzia siasa kama mfumo unaotambulika na kukubalika na watu wote katika kuratibu rasilimali zote za taifa, iwe ni watu, fedha, maliasili zote zinazohusika kama maji, ardhi, madini, wanyama pori na misitu katika kumnufaisha mwananchi mmoja mmoja na hatimaye kuleta maendeleo endelevu kwa jamii ya watu wote kama Taifa.

Vile vile katika swali hili ningependa sana walengwa wa kwanza kujiuliza swali hili wawe wananchi wote  wa Tanzania lakini hasa ningependa kuwatambua kwa kuwaweka katika makundi yafuatayo:- Kundi la kwanza ni la wananchi wanaojihusisha na siasa katika vyama vya siasa iwe ni chama tawala au vyama vya upinzani. Kundi la pili ni la wananchi wasiojuhisha na vyama vya siasa ila wao hupenda kufuatilia nyendo za kisiasa na kuishia kutoa maoni na mitazamo yao kwa namna mbalimbali. Kundi la tatu ni la wananchi wasiojua nini kinaendelea katika siasa nchini mwao lakini hujikuta wakishiriki katika michakato ya kisiasa bila ya wao kujua, kwa mfano kutakiwa kupiga kura huku akiwa hajui atakayempiga kura ni nani na atafanya nini endapo atachaguliwa kuwa kiongozi ama wa kata, jimbo au Urais.

Siasa kama mfumo nilioulezea hapo juu kwa ufupi huwa na athari chanya au hasi katika maisha ya kila mwananchi wa nchi husika. Kuufahamu mfumo wa kisiasa wa nchi yako ama kutokuufahamu hakuwezi kuzuia uwezo wa mfumo huu kuathiri maisha yako kwa namna zote mbili yaani kwa faida au hasara. Ni vyema kila mwananchi akafahamu kuwa siasa ni maisha yake na maisha yake ni siasa. Hakuna jambo litakalofanyika katika ngazi ya kijiji, kata, wilaya, mkoa na taifa lisilohusisha utashi wa kisiasa. Hivyo utashi wa kisiasa katika ngazi zote za uongozi wa nchi hauepukiki na kila mwananchi anawajibika kujihusisha na mfumo wa kisiasa ili adhma ya kutumia mfumo wa siasa katika kuratibu rasilimali za taifa umnufaishe yeye binafsi na hatimaye kuleta maendeleo endelevu kwa jamii ya watu wote kama Taifa.

Nchi yetu inajivunia kuwa na historia ya aina yake katika nyanja za kisiasa. Kwa ufupi kabisa nitagusia mtiririko wa kihistoria huku nikitumia maana ya siasa kama “mfumo unaotambulika na kukubalika na watu wote katika kuratibu rasilimali zote za taifa, iwe ni watu, fedha, maliasili zote zinazohusika kama maji, ardhi, madini, wanyama pori na misitu katika kumnufaisha mwananchi mmoja mmoja na hatimaye kuleta maendeleo endelevu kwa jamii ya watu wote kama Taifa”. Kabla ya kupata uhuru wa kisiasa, nchi yetu ilikuwa chini ya mfumo wa kisiasa wa wakoloni ambao wao kama ilivyo desturi ya mfumo wa kisiasa waliutumia kujinufaisha wao na watu wao waliokuwa ughaibuni. Hali tukiwa tunatawaliwa hatukuweza kunufaika na mfumo wa siasa za kikoloni kwa kuwa huo ulilenga kuwanufaisha wananchi wao kwa njia za unyonyaji. Hapo ndipo harakati za kudai “uhuru wa kisiasa” (political liberation) zilipamba moto na hatimaye nchi yetu ikatunukiwa uhuru wa kisiasa Desemba 9 mwaka 1961.

Muelekeo wa kisiasa ukabidilika mara baada ya nchi kupata uhuru wa kisiasa kutoka kuwa na vyama vingi katika utawala wa kikoloni na kuwa na chama kimoja cha siasa katika utawala mpya wa kiafrika. Hapa agenda yetu sisi ikawa ni kuijenga nchi kwa dhana ya kuweka umoja na mshikamano na kuondoa ukabila na udini ulichochewa na wakoloni ili waweze kututawala vizuri. Agenda hii ilikuwa nzuri kwa wakati ule, hasa ukizingatia kuwa wakoloni walitumia kamchezo walichokaita kwa lugha yao kuwa “devide and rule”. Lakini sisi agenda yetu ya kisiasa ilibidi ibadilike ili iweze kukidhi haja ya wananchi wote kunufaika na rasilimali za taifa. Hivyo mfumo wa vyama vingi endapo ungepewa nafasi ungeweza kuongeza kasi ya kutugawanya na hivyo kukosa umoja na mshikamano ambao ungetumika kuijenga nchi yetu ili itunufaishe. Mfumo wa chama kimoja ulikuwa una kasoro zake ambazo kwa wakati huo hazikuwa nyingi ukilinganisha na faida zake, ambazo hadi leo hii matunda yake tunayaona kwa Watanzania wote kuishi kwa upendo, kitu ambacho nchi nyingine zinazotuzunguka hawana.

Dhamira na agenda ya kisiasa wakati wa mfumo wa chama kimoja ulio ongozwa na hayati Baba wa Taifa ulikuwa sahihi kwa wakati wake. Miaka ya 1980 kukatokea msukumo na shinikizo kutoka kwa waliokuwa wakitutawala wakitutaka kurudi kwenye mfumo wa vyama vingi kwa hoja kivuli za kutimiza dhana ya uwajibikaji na kuweka demokrasia, kukatufanya kurudi na kuridhia mfumo ambao wao waliutumia kututawala wakiwa huku kwetu na sasa wangependa kuutumia huku wakitutawala kutokea kwao (ughaibuni). Uamuzi wa kuingia katika mfumo wa vyama vingi vya siasa uliambatana na mapitio ya katiba ya nchi na sheria zake ili kuzifanya ziweze kukidhi haja ya wakati na kuuratibu mfumo wenyewe, kazi iliyofanywa vyema na tume ya marehemu Jaji Francis Nyalali ambayo ilizitamka sheria takribani 40 kama “bad laws” ambazo zinahitaji mabadiliko ya haraka ili mfumo wa vyama vingi vya siasa uwe na manufaa kwa wananchi wote. Kazi ya kurekebisha au kuzifuta sheria hizi ili zikidhi haja ni hoja ya kisheria sana ambayo huenda naweza nisiitupie macho kwa kina kama ambavyo wangeweza kufanya wanasheria, ila ukweli kuwa chochote katika kufanya mabadiliko ya sheria hizi hakijafanyika sitaacha kuusema ili wanaohusika na kulitatua hili wakumbuke kufanya hivyo pamoja na kuwa ni miaka zaidi ya 15 tangu mapendekezo hayo yatolewe. Kuanzia kwenye hoja hii tunaweza kuanza kuhoji uhalali wa kile tunachosema kupitia vyama vyetu vya siasa kama “agenda” zetu tukianzia na chama tawala ambacho ndicho kilichoishika dola kwa sasa na ndio chama kile kile kilichoishika dola wakati mapendekezo ya tume ya Marehemu Jaji Francis Nyalali yalipotolewa. Wakati huo huo tukijiuliza ni zipi agenda za vyama vya upinzani vyenye ushawishi mkubwa hivi sasa katika vyombo vya maamuzi kama bunge na ambavyo vimeweza kuvumilia kuwa na mfumo wa vyama vingi ndani ya “sheria 40” ambazo zilitamkwa kuwa ni “bad laws” na iliyokuwa tume ya Mheshimiwa Nyalali?. Tunakuja kugundua kuwa agenda “nambari moja” ya kila chama cha siasa ni kushinda uchaguzi mkuu na kuunda dola, jambo lililoshuhudiwa katika miaka 15 iliyopita huku chama tawala kikiibuka na ushindi mkubwa katika viti vya madiwani, ubunge na urais na kuunda dola. Huku vyama vingine vya siasa vinavyotamkwa kuwa vyenye ushawishi mkubwa vikufuatia nyuma na kushika mkia. Baada ya kushindwa kwa “agenda nambari moja” ya kushinda uchaguzi mkuu na kuunda dola kwa vyama vya upinzani tangu mwaka 1995, 2000 na 2005 tumeshuhudia “agenda nambari mbili” ya vyama vya upinzani ya “kuking’oa chama tawala” ikipamba moto huku ikisindikizwa na mbwembwe za kisiasa za kuunda umoja wa vyama vya upinzani agenda iliyoonekana kufeli kutokana na kila chama cha upinzani kuwa na “agenda nambari tatu” inayofanana na “agenda nambari mbili” ya chama tawala ambayo hiyo inalenga kuuendelea kuishika dola kwa udi na uvumba ili kuendela kula keti ya Taifa kama ilivyodhirika kwa wale waliokumbwa na kashfa za ufisadi kama rada, Richmond, ndege ya rais, majengo pacha ya benki kuu na Buzwagi. Agenda nambari mbili ya vyama vya upinzani awali ilionekana kuwa na utashi wenye maslahi ya Kitaifa lakini masikitiko yangu makubwa ni kuwa agenda hii imekumbwa na dhoruba ya “devide and rule” na sasa dhamira ya upinzani kuunganisha nguvu ili kuking’oa chama tawala haitafanikiwa mpaka watakapotambua kuwa “agenda zao” zote haziendani na matakwa ya wananchi wa Tanzania. Matakwa ya wananchi wa Tanzania ni yepi? Tukiligundua hili ni rahisi kwa agenda nambari mbili ya vyama vya upinzani ikafanikiwa na hatimaye kuking’oa chama tawala. Na chama tawala kitajifunza kutoka kwa upinzani juu ya nini wananchi wanataka.

Mimi naona vyama vyetu vya siasa havina agenda sahihi kwa wananchi na taifa kwa ujumla. Kama agenda ni “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu”(Rapid increase of sustainable development) kwanini ndoa ya vyama vya upinzani ilivunjika? Kama agenda ni “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu” kwa nini zitumike mbinu chafu za kushinda uchaguzi na kuuita ushindi wa kishindo ili muendelee kula keki ya Taifa? Ipo haja ya vyama vya siasa kujipitia upya na kutoa kipaumbele kwa agenda yenye maslahi ya kitaifa ya “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu”. Hii agenda ikitupiwa macho kwa makini itatusaidia.Kama lengo letu likawa moja yaani kuleta kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu, ninayo rai moja tu kwa vyama vya upinzani. Tumeshuhudia vyama vya upinzani vikishindwa vibaya katika chaguzi zilizopita. Mwaka huu(2010) pia kuna uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na urais na kitu cha kushangaza tayari vyama viwili vya upinzani kati ya vyama vilivyowahi kufunga ndoa huko nyuma kila kimoja kimetangaza nia ya kusimamisha mgombea wake wa Urais katika uchaguzi wa Octoba 2010. Ni uamuzi mzuri tena wa kidemokrasia lakini unatufanya tuendelee kuhoji legitimacy ya agenda za coalition mliyoiunda na iliyofeli. Kama agenda ya vyama vya upinzani ni “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu” nawashauri mvunje vyama vyenu vyote na muunde angalau chama kimoja chenye nguvu kitakachosimamisha mgombea mmoja wa kiti cha urais na mkitumia mwanya huo kuwa na wabunge wengi katika viti vya ubunge ili kupush agenda ya “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu . Katika hili kama agenda zenu zitabakia kuwa zile nilizozitaja hapo juu pindi mnapokuwa kwenye vyama vyenu, napenda nitoe tahadhari kuwa yanaweza kuwafika kama yale yaliyoikumba PNU kule Kenya na baadaye kuleta mvutano wa kugawana madaraka na ODM kama ilivyo kwa ZANU-PF na MDC kule Zimbwabwe, serikali ambazo hazina tija kwa Taifa kwa sababu zinatanguliza maslahi binafsi mbele badala ya maslahi ya Taifa. Ni furaha yangu kuona kuwa kila Mtanzania anayeshiriki katika siasa na atakayepiga kura katika uchuguzi mkuu ujao mwezi Octoba 2010 kwa namna yoyote ile anaipa kipaumbele agenda ya “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu” kwa maslahi ya kizazi cha sasa na kile kijacho. Wakati huo huo kila mmoja hali akitafakari makala hii ajiulize “kwani katika siasa mimi agenda yangu ni ipi?” Ningependa sana agenda yako iwe “kuongeza kasi ya maendeleo na kuyafanya yawe endelevu” kwa maslahi ya kizazi cha sasa na kile kijacho. Mungu wabariki Watanzania wawe na nguvu ya kuliona hili.Mungu Ibariki Tanzania. Mungu Ibariki Afrika, watu wake na viongozi.

Monday, February 22, 2010

ExVIBE organized the first workshop in Songea

Extra Vision 2020 and Beyond (ExVIBE) in collaboration with the Labour Administration and Inspection office of Songea which is an office under the Ministry of Labour, Employment and Youth Development conducted the students workshop on Career Identification and University Course Selection at Songea Club Multimedia Hall on 20th February 2010.
          The Workshop was attended by more than 80 students from different Advanced level Secondary Schools of Songea Municipal. The schools include Songea Boys Secondary School, Songea Girls Secondary School, Ruhuwiko High School, Kigonsera High School and Beroya Secondary School. The workshop was officially opened by acting Regional Administrative Secretary (RAS) of Ruvuma Region. The acting RAS opening speech stressed important issues on employment policy of Tanzania. He said that “65 per cent of the total labour force in Tanzania is youth aged 18-35 thus being among the social group which contributes a lot in the development of this nation.
         Speaking of the workshop itself the organizer and facilitator of that workshop Mr. Frederick Fussi said that “the goal of this workshop is to widen the students understanding on the employment industry nationally and internationally, however the purpose of the workshop is also targeting at improving awareness on Career Identification and University Course Selection”
        The workshop outputs were expected to be Increased information on carrier identification, Increased awareness on the employment industry, Increased awareness on the university course selection, Increased youth empowerment on self employment.
        In order to make this a reality the different renowned and experienced resource persons in Songea presented papers. Eng. Mrs. Mwapongo presented a paper on “self employment and entrepreneurship”. Eng. Kazimoto presented a paper on “Southern Development Opportunities”, Accountant Phinias Opanga presented a paper on “Human Resource Management”, a renowned journalist from TBC Mr.Gerson Msigwa presented a paper on “employment opportunities in Information and Communication Technology”. Other presenters include a labour officer Mr. Oddo Egino Hekela presented a paper on “employment industry” while Frederick Fussi presented papers on “self awareness and university course selection.” The workshop took the duration of one day.

Tuesday, February 16, 2010

UONGOZI NI MAONO

Sifa ya Kiongozi yeyote yule duniani katika nyanja za kila namna ni sharti awe amebeba maono ndani yake ili aweze kuongoza au kuliongoza kundi kwa usahihi mkubwa. Labda tujiulize kwa nini kundi linahitaji kuongozwa?

Hakuna dereva anayeweza kuendesha gari vizuri asipoifahamu barabara aiendeayo au kuufahamu mwisho wa safari yake. Kadhalika kiongozi naye ni lazima afahamu watu anaowaongoza na kutambua kule anakowapeleka. Tunamfananisha kiongozi mzuri na dereva stadi anayelifahamu gari lake kwa ufasaha na kuweza kulichunguza kwa makini na kabla ya hayaanza safari yake hujenga picha akilini mwake juu ya kule anakotakiwa kulifikisha gari lake kwa usalama wa hali ya juu. Dereva huyu lazima kwa namna moja ama nyingine atakuwa amepakia abiria au mizigo ndani ya gari lake. Uwezo wa dereva kupiga picha ya safari nzima tungu mwanzo wa safari hadi mwisho wake humfanya dereva kuwa na sifa ya maono. Hatumtegemei dereva huyo kufanya tofauti na maono yake. Maono yake ni kuliendesha gari lake kupitia barabara fulani kwa mwendo fulani na kufika sehemu husika ndani ya muda uliopigiwa mahesabu. Kuzifahamu changamoto zitakazomkabili njiani wakati wa safari nayo pia ni sifa ya dereva huyu mzuri mwenye maono.

Kadhalika kwake kiongozi mwenye maono huwafahamu watu wake vizuri, huzijua changamoto za watu wake na yeye hufahamu namna bora ya kuzikabili hizo changamoto ili aweze kulipigisha hatua kundi lake. Kiongozi bora ni mwenye maono mithili ya mchungaji wa kondoo. Mchungaji wa kondoo huwatoa zizini asubuhi hali akifahamu aina ya malisho sahihi kwa ajili ya afya ya kondoo wake. Hufamu vyema mto ule wenye maji safi na salama ambayo kondoo wake watayanywa wakiwa malishoni. Wanyang’anyi wajaposogelea kundi la kondoo wake yeye husimama kidete kuwatetea kwa kuwa ana maono ya kuwarudisha salama katika zizi lile lile alilowatoa asubuhi.

Uongozi ni maono, pasipo maono uongozi huwa mgumu na mafanikio habakia kuwa ndoto miongoni mwa kundi ama watu wanaoongozwa. Kiongozi hubeba maono ambayo hushikwa na wale anaowaongoza. Uwezo wa kundi kuyashika maono ya kiongozi wao ndio uwezo wa kundi kufanikiwa na kuwa salama nyakati zote. Wapo watu ambao sio viongozi lakini wanaongoza. Watu wa namna hii hutawaliwa na nyakati zisizokuwa na mafanikio yaliyo dhahiri. Viongozi hawa huwa na sifa ya kukosa maono na uzoefu anonesha kuwa viongozi hawa huliyumbisha kundi wanaloliongoza. Uongozi ni maono, maono hayo hubaki kuwa msaada mkubwa kwa kuwa watu au kundi linaloongozwa na kiongozi mwenye maono hufanikiwa kwa kasi ya ajabu kwa sababu imo siri kubwa ndani ya kiongozi aliyebeba maono sahihi na maono hayo yakashikwa na kundi lake.

Friday, January 1, 2010

TAIFA LENYE MAONO NA WATU WENYE MAONO


Ukuaji wa Taifa lolote lile duniani unategemea na aina ya maono ya watu au wananchi wanaoishi ndani ya hilo Taifa. Maono ni uwezo wa mtu kuona mambo yajayo kabla ya wengine, kuyaona sana kuliko wengine na kuona mbali zaidi ya wengine.


Ili Taifa likue linahitaji kuwa Taifa lenye maono ya hali ya juu. Na ili maono yawepo panahitajika wawepo watu wachache na sio wote wanaoweza au wenye uwezo wa hali ya juu wa kuona na kubeba maono ya Taifa hilo. Kwa mfano kabla Tanganyika haijapata uhuru palikuwepo na watu wachache wenye uwezo mkubwa wa kuona mbali na kuweza kubeba maono ya Taifa. Watu hawa ndio waliokuwa viongozi na vinara wa kuung’oa utawala Kiingereza katika ardhi ya Watanganyika na kuamua kuunda upya Taifa lao.
 Kimsingi zipo awamu nne tangu Taifa letu lipate uhuru. Katika awamu hizi nne kumekuwepo na matarajio ya kuwa tungekuwa na watu wachache wenye maono ya kulijenga Taifa letu kama ilivyokuwa kwa kipindi cha Mwl. J.K. Nyerere. Mfano mzuri Mwl. Nyerere alikuwa mtu mwenye maono. Mwalimu aliamini katiaka maono yake kwa Taifa na kuwa mstari wa mbele kuongoza Watanzania wenzake. Si kweli kwamba Mwl. Nyerere aliweza kuyafanya mambo yote peke yake la hasha alikuwa na wasidizi wake wa Karibu ambao nao pia waliamini ndani ya maono ya Mwalimu na kuyashika hayo maono. Kwa mantiki hii sasa tunagundua kuwa Mwalimu alikuwa na maono na wasaidizi wake walijifunza ama kuyashika au kuyakataa. Enzi hizo ili Taifa likue ilitegemea ni namna gani wasaidizi wa Mwalimu walikubali kuyashika maono na kuyatendea kazi. Katika kipindi hicho wapo wale walioyashika maono na kuyatendea kazi na wapo baadhi ambao hawakuona umuhimu wa kuyashika maono.

Uwezo wa Taifa kukua unategemea ni namna gani watu wa Taifa hilo wanayashika maono ya kiongozi wao na kuyatendea kazi. Ili Taifa likue linahitaji maono sahihi ya kiongozi wa Taifa. Si kila mtu tunayemwita kiongozi anaweza kubeba maono ndani yake. Na si kila mtu anaweza kubeba maono. Ili kuweka uwiano katikati ya Taifa lazima awepo mtu mmoja ambaye ndani yake anakuwa amebeba “maono ya Taifa lake”. Maono ya Taifa huanza ndani ya mtu mmoja na watu wa Taifa lake huwa watu wenye maono kwa sababu tu wameyashika maono ya mtu mmoja miongoni mwao. Kukikosekana mtu mmoja mwenye maono Taifa hupitia katika vipindi vigumu tofauti na aina ya ugumu unaojitokeza endapo Taifa lina mtu aliyebeba maono na wengine kuyashika. Taifa letu Tanzania linahitaji “maono sahihi” kutoka kwa “mtu sahihi” na Watanzania wote wanahitaji kuyashika maono hayo ili Taifa lao lipige hatua.

Taifa letu Tanzania bado linatembea ndani ya maono ya mtu mmoja ambaye bahati nzuri alishamaliza kazi yake na hivyo maono hayo kufikia ukomo kiuhai. Kuna “maono hai” (active vision) na “maono yaliyokufa” (dormant vision). Tanzania kwa sasa haina “maono hai”. Ni vigumu mtu kuamini kama Tanzana ya sasa haina “maono hai” Lakini ukweli unabakia kuwa Taifa letu kwa sasa halina maono hai. Huhitaji kuwa na elimu kubwa kutambua kuwa Taifa linatembea ndani ya “dormant vision”. Chunguza kasi ya ukuaji wa kiuchumi kwa mtu mmoja mmoja na wa Taifa na kasi ndogo Maendeleo ya jamii utagundua kuwa hatua tulipo sasa ilibidi tuipige zaidi ya miaka 30 iliyopita.Tunaweza kujivunia hatua ile tuliyoipiga sasa, vyema, lakini hatustahili kujivunia kwa sababu Tanzania ni zaidi ya mafanikio yote tuliyonayo sasa. Tanzania haistahili kuwa ilipo sasa. Ipo njia sahihi ya kuifikisha Tanzania inapotakiwa kuwapo. Upo umuhimu wa kila Mtanzania kugundua kuwa hatustahili kuwa hapa tulipo. Tunayo stahili yetu. Na ili kuifikia stahili yetu sharti tukubali kulipia gharama za kuwa na maono hai(active vision). Na huu ndio mwanzo mpya wa maono hai (the new beginning of an active vision).